Friday, December 16, 2016

TUTAFUTA NGO ZOTE ZINAZOFANYA KAZI KINYUME CHA SHERIA NA KATIBA YA NCHI- MAJALIWA

WAZIRI MKUU Kassim Majaliwa amesema Serikali itazifutia usajili Taasisi zote zisizokuwa za Kiserikali (NGO’s) zilizoko kwenye Tarafa ya Loliondo zinazofanyakazi kinyume na katiba zake na sheria ya nchi ambapo ametoa miezi sita zijitathimini kama zinafanya kazi ya kuhudumia jamii au la.

Pia ameahidi kumpeleka Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) katika Taraha hiyo ya Loliondo kwa lengo la kuzifanyia ukaguzi NGO hizo ili kubaini kiasi cha fedha wanazopata kama zinalingana na matokeo ya kazi za kijamii inazofanya katika Tarafa hiyo.

Waziri Mkuu alitoa kauli hiyo leo (Alhamisi, Desemba 15, 2016) wakati akizungumza na Wakurugenzi wa NGO na watumishi wa Halmashauri ya Wilaya ya Ngorongorokwenye ukumbi wa Halmashauri hiyo akiwa katika ziara ya kikazi mkoani Arusha.

Amesema NGO nyingi zimekuwa zikipata bajeti kubwa ya fedha lakini masuala ya maendeleo wanayoyafanya katika eneo hilo hayalingani na bajeti halisi wanazopata.”Loliondo pekee kuna NGO zaidi ya 30 ila zilizokuwa ‘active’ ni 15 tu kuna nini Loliondo? Na baadhi yake zinafanya kazi ya kuchochea eneo hili lisiwe na amani,”.

Waziri Mkuu ameongeza kuwa “watu wote wanaoshirikiana na NGO hizo zinazochafua taswira ya nchi tutawashughulikia. Mnawavalisha watoto kandambili zilizotobona na miguu michafu kisha mnawapiga picha mnazituma kwenye mitandao na kusema umasikini wa Tanzania ndio huo. Hatutawavumilia watu wa namna hii,” amesisitiza.                                                    

Amesema NGO nyingi zimekuwa zikilalamikiwa kutokana na kufanya kazi kinyume na mikataba yake ya usajili na miongoni mwa NGO hizo ni pamoja na PWC inayopata sh. bilioni 2.5 kwa mwaka, UCRT inayopata sh. bilioni 1.5 kwa mwaka, Oxfarm Tanzania inayopata sh. bilioni 1.7 kwa mwaka.

“Nitafuatilia kwa karibu kuona kazi wanazozifanya kwani zinapata fedha nyingi kwa mwaka. Lazima tujenge nidhamu kwa wote wanaopata fedha kwa lengo la kuisaidia jamii. Wote wanaojihusisha na shughuli nje ya mikataba yao wabadilike ndani ya miezi sita. Wafuate kanuni, sheria na taratibu za nchi,” amesema.

Amesema Serikali haiwezi kufanya kazi bila ya wadau ila haiitaji wadau wanaofanya mambo kinyume cha taratibu, ambapo amezitaka NGO hizo kusajiliwa na Wakala wa Usajili wa Kampuni (BRELA) ili ziweze kutambulika kisheria na ofisi zake kujulikana badala ya hivi sasa kuwa na ofisi za mifukoni.

Awali, Waziri Mkuu alizungumzia na wananchi wa kijiji cha Ololosokwan ambapo alisema  mgogoro wa ardhi kati ya wananchi wa Tarafa la Loliondo na wawekezaji unaolikabili eneo hilo Waziri Mkuu mesema Serikali itahakikisha mgogoro huo uliodumu kwa muda mrefu unamalizika haraka.

Aidha, amemwagiza Mkuu wa Mkoa wa Arusha, Bw. Mrisho Gambo kukutana na uongozi wa wilaya ya Ngorongoro na kamati ya wananchi iliyoundwa kwa ajili ya kuboresha uhifadhi ili kumaliza mgogoro huo na kisha kumpelekea taarifa.

“Haiwezekani Waziri Mkuu aje kumaliza mgogoro wa ardhi Loliondo wakati kuna viongozi hapa. Mimi nimemuagiza Mkuu wa mkoa aje akutane na wawekezaji na wananchi ili kuzungumza na kuupatia ufumbuzi mgogoro huu na atakayeshindwa ndiye nitakayemshughulikia,” amesema.

Amesema Serikali itahakikisha migogoro ya ardhi inamalizika nchini ili kuwawezesha wananchi kufanya shughuli zao kwa amani na utulivu. “Naomba tushirikiane katika kutatua changamoto hii ya migogoro ya ardhi kwani suala hili limeahidiwa katika ilani ya uchaguzi ya CCM,”.

Wakati huo huo, Waziri Mkuu amepiga marufuku tabia ya baadhi ya wananchi kuingiza ng’ombe kiholela kutoka nje ya nchi kwa kuwa kitendo hicho kinachangia kuwepo kwa migogoro ya ardhi.
Katika kuhakikisha suala hilo linadhibitiwa Waziri Mkuu amemtaka Mkuu wa wilaya hiyo, Bw. Rashid Taka kwa kushirikiana na kamati ya ulinzi na usalama ya wilaya hiyo kuimarisha ulinzi katika mipaka kwa kuongeza doria ili kudhibiti uingiaji holela wa mifugo.

Naye Waziri wa Maliasili na Utalii, Profesa Jumanne Maghembe alisema  eneo la Loliondo ni muhimu sana kwa ajili ya ikolojia ya wanyama pamoja na maji kwani hifadhi ya Serengeti inategemea zaidi eneo hilo.

 


EmoticonEmoticon

Note: Only a member of this blog may post a comment.