Tuesday, December 6, 2016

KAMPUNI ZA WATUMISHI ZISIPEWE ZABUNI NDANI YA HALMASHAURI WANAZOZITUMIKIA-MAJALIWA

WAZIRI MKUU Kassim Majaliwa amemuagiza Mkuu wa Wilaya ya Karatu, Bi. Theresia Mahongo kuhakikisha kampuni zinazomilikiwa na madiwani na watumishi wa halmashauri hiyo hazipewi  zabuni zinazotolewa katika maeneo yao kwa ajiliya  kuepusha migongano ya kimaslahi.

Ametoa agizo hilo leo (Jumatatu, Desemba 5, 2016) wakati akizungumza na watumishi wa halmashauri ya wilaya ya Karatu mkoani Arusha katika ukumbi bwalo la  Shule ya Sekondari ya Wavulana ya Karatu akiwa katika ziara yake ya kikazi mkoani hapa.

"Hauzuiliwi kufanya biashara ili mradi kampuni yako isifanye kazi katika halmashauri ambayo wewe unaitumikia na una nguvu nayo ili kuepusha migongano ya kimaslahi kwani miradi yote utajilundikia," amesema.

Pia amewataka Wakuu wa Idara katika halmashauri hiyo walisaidie Baraza la Madiwani katika kubaini vyanzo vipya vya mapato kwa lengo la kuongeza mapato ya halmashauri yao.

Wakati huo huo Waziri Mkuu amewataka watumishi wa halmashauri wa umma  kujitathmini na kujiridhisha kama wanafuata misingi ya utumishi katika utendaji kazi wao wa kila siku. Amewasisitiza  wawatumikie wananchi kwa uadilifu na uaminifu mkubwa.

"Hatuhitaji kuwa na mtumishi mvivu, asiyewajibika, mwizi, mla rushwa na asiyekuwa muadilifu mahali pa kazi.
Na  atakayeona ameshindwa kutunza na kusimamia fedha za miradi ya maendeleo ya wananchi atoe taarifa hatutaki watu kufanya kazi kwa mazoea," amesema.

Waziri Mkuu ameongeza kuwa " watumishi wa umma lazima mbadilike na muwe na nidhamu ya kazi. Muache malalamiko fanyeni kazi na msitafute  sympathy (huruma) kutoka kwa watu kwani Serikali haitamuonea mtumishi yeyote ," amesema.

Amesema katika baadhi ya ofisi za Serikali kuna ugonjwa wa watumishi wanapoona wageni wamelifika kwa ajili ya kupatiwa huduma wanawapita bila ya kuwasikiliza. " sasa hatutaki watumishi wa namna hiyo, Jukumu lako ni kumtumikia Mtanzania na tunataka kuona mabadiliko. Hatutaki kuona watu wakizubaa maofisini,".

Waziri Mkuu amesema Serikali ikikuta wananchi wanalalamika kutokana na kutoridhishwa na  huduma zitolewazo na watumishi wa umma itahakikisha watumishi hao wanachukuliwa hatua. Serikali ni ya Watanzania wote hivyo lazima wahudumiwe vizuri bila ya kujali uwezo wao kifedha wala itikadi zao za kidini na kisiasa.


EmoticonEmoticon

Note: Only a member of this blog may post a comment.