Thursday, December 22, 2016

KANISA LA EAGT LACHANGIA SH. MILIONI 10 KWA WALIOPATWA NA MAAFA KAGERA

WAZIRI MKUU Kassim Majaliwa amepokea fedha taslimu sh. milioni 10 kutoka Kanisa la Evangelistic Assemblies of God Tanzania (EAGT) zikiwa ni msaada kwa ajili ya watu waliopatwa na maafa kutokana na tetemeko la ardhi mkoani Kagera.

Makabidhiano ya mchango huo yamefanyika leo mchana (Alhamisi, Oktoba 22, 2016) kwenye Makazi ya Waziri Mkuu, Oysterbay, jijini Dar es Salaam.

Akikabidhi mchango huo, Askofu Mkuu wa Kanisa la EAGT, Dk. Brown Mwakipesile amesema kanisa hilo limeona lina wajibu wa kuisadia Serikali kuwapunguzia machungu watu waliopatwa na maafa kutokana na tetemeko la ardhi lililotokea mkoani Kagera, Septemba 10, mwaka huu na kusababisha vifo vya watu 17.

“Tumeona ni vema kanisa la EAGT lishiriki kuisadia Serikali kuwafariji wananchi waliopata maafa kutokana na tetemeko hilo. Tumeona ni wajibu wetu kwa sababu waliopatwa na maafa ni watu wetu wote. Tunawaombea wote waliopatwa na shida waweze kupata nafuu mapema zaidi,” amesema.

Askofu Mkuu Dk. Brown ametumia fursa hiyo kuipongeza Serikali kwa kusimamia vema suala hilo tangu lilipotokea hadi sasa na kuongeza kuwa wanamuomba Mwenyezi Mungu awape nguvu viongozi wa Serikali ya awamu ya tano ili waweze kutimiza majukumu yao ipasavyo.

“Ukiacha hili la tetemeko, tumeona jinsi Serikali ilivyosimamia vizuri suala la madawati hadi sasa kuna baadhi ya maeneo wamevuka hadi malengo. Tunamshukuru Mheshimiwa Rais Magufuli na Serikali nzima kwa kusimamia jambo hilo vizuri,” amesema.

Amesema kanisa hilo linatoa shukrani nyingi kwa Mheshimiwa Rais Dk. John Pombe Magufuli kwa jitihada zinazofanywa na Serikali yake kukabili mambo mbalimbali yanayowagusa wananchi walio wengi.

Akitoa shukrani kwa Baba Askofu Mwakipesile na viongozi wa kanisa hilo aliombatana nao, Waziri Mkuu ameahidi kuwa Serikali itahakikisha michango hiyo inafikishwa Kagera kwa walengwa. “Nawashukuru sana kwa jinsi mlivyoguswa na kuamua kuwachangia wenzetu waliopatwa na maafa, tutahakikisha inawafikia walengwa,” amesema.

Waziri Mkuu amesema anawashukuru sana viongozi wa dini zote kwa jinsi wanavyoisadia Serikali kuwahudumia wananchi kupitia sekta mbalimbali. “Tunatambua juhudi zinazofanywa na taasisi za dini zote kuunga mkono juhudi za Serikali, tunafarijika mno na tunawashukuru sana,” ameongeza.

Amemuomba Askofu huyo pamoja na viongozi wengine wa dini wawaombee kwa Mungu viongozi waliopo madarakani ili awape hekima na busara na awawezeshe kuwaongoza vema Watanzania.

Tetemeko hilo la ardhi liliharibu miundombinu ya barabara, shule, zahanati na kujeruhi watu 440. Pia lilisababisha nyumba 2,063 kuanguka huku nyingine 14,081 zikiwa katika hali hatarishi na 9,471 zikipata uharibifu mdogo huku wananchi 126,315 wakihitaji misaada mbalimbali.


EmoticonEmoticon

Note: Only a member of this blog may post a comment.