Saturday, December 24, 2016

MAMA MAJALIWA ATOA MISAADA KWA WATOTO YATIMA

MKE wa Waziri Mkuu Mama Mary Majaliwa ametoa msaada wa vitu mbalimbali kwa makundi ya watoto yatima jijini Dar es Salaam ili kuwawezesha kufurahia sikukuu za mwisho wa mwaka.

Mama Majaliwa ametoa msaada huo leo (Jumamosi, Desemba 24, 2016) katika vituo vitatu vya CHAKUWAMA kilichopo Sinza, HISANI kilichopo Kigamboni na CHAMAZI kilichopo Mbagala.

Akikabidhi msaada huo ikiwemo mchele, sabuni, mbuzi, juisi na soda, Mama Majaliwa amesema ameona ni vema atoe msaada huo kwa watoto hao ili na wao waweze kufurahia sikukuu za mwisho wa mwaka kama ilivyo kwa watoto wengine.

Pia ametoa wito kwa makundi mbalimbali yenye uwezo katika jamii wawe na moyo wa kusaidia makundi yenye uhitaji.

Kwa upande wao, walezi wa vituo vya kulelea watoto yatima vya CHAKUWAMA na HISANI wamemshukuru mke wa Waziri Mkuu kwa msaada huo huku baadhi ya watoto wakisema msaada huo umewapa faraja kubwa.

Mlezi wa kituo cha CHAKUWAMA, Bibi Saida Hassan mbali ya kushukuru kwa msaada huo, amewaombea kwa Mwenyezi Mungu awape afya na nguvu za kuendelea kuwatumikia vizuri Watanzania.

Naye Mlezi wa kituo cha HISANI, Bi. Hidaya Mutalemwa ameiomba jamii iendelee kuyakumbuka makundi yenye uhitaji kwani bado yanakabiliwa na changamoto nyingi za kufanikisha ndoto zao ikiwemo kupata elimu.


EmoticonEmoticon

Note: Only a member of this blog may post a comment.